Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Marekani yaishambulia Iran, baada ya wanajeshi wake kuuawa

Marekani imeanzisha mashambulizi mapya dhidi ya Iran baada ya wanajeshi wake wawili kuuawa nchini Jordan katika shambulio lililotekelezwa na Iran

Moja kwa moja

Na Beldeen Waliaula

  1. IAEA yaanzisha uchunguzi baada ya Marekani kushambulia kituo cha nyuklia Iran

    Shirika la Kimataifa la Nishati ya Atomiki (IAEA) limetangaza kuwa linafanya uchunguzi kuhusu taarifa za shambulio la usiku wa kuamkia leo dhidi ya eneo ambalo kiwanda cha nyuklia cha Darkhovin, kilikuwa kinajegwa nchini Iran.

    Shirika hilo limesema kituo hicho kilikuwa bado katika hatua za kwanza za ujenzi, na walipofanya ukaguzi wao wa mwisho, hakukuwa na nyenzo za nyuklia zilizokuwepo katika eneo hilo.

    Shirika la Nishati ya Atomiki la Iran limeshutumu Marekani kwa kushambulia kituo kilichokuwa kikijengwa cha nyuklia cha Darkhovin.

    Katika taarifa yake, shirika hilo limesema kuwa Marekani, imekiuka sheria za kimataifa kwa kushambulia kituo hicho.

    Soma pia:

  2. Zaidi ya wanajeshi 50 wauawa na kundi la waasi nchini Mali

    Wapiganaji wa waasi wa Tuareg nchini Mali kwa kushirikiana na wanamgambo wengine wenye itikadi kali, wamevamia msafara wa jeshi la Mali katika eneo la Gao, na kuua angalau wanajeshi 50, kulingana na maafisa waliozungumza na shirika la habari la AFP.

    Kwa kujibu shambulio hilo,jeshi la Mali limesema lilitekeleza mashambulizi ya anga yaliyowalenga wapiganaji hao na kuwaua takriban wapiganaji 20, kuharibu magari manne ya kubeba wapiganaji na kuangamiza ngome tatu za waasi karibu na eneo la Tabrichat, hatua iliyowezesha msafara wa jeshi hilo la Mali kuendelea na safari yake.

    Hata hivyo, maafisa wameiambia AFP kuwa idadi ya waliouawa ni zaidi ya wanajeshi 50, huku angalau wanajeshi 24 wakidaiwa kutekwa na waasi hao, na kufanya hili kuwa moja ya mashambulizi mabaya zaidi dhidi ya jeshi la Mali katika miaka ya karibuni.

    Kundi la The Azawad liberation front, linaloshirikiana na kundi la wanamgambo la JNIM, limedai kuhusika na shambulio hilo, ilamadai hayo hayajathibitishwa.

    Kwa sasa hali ya usalama kaskazini mwa Mali inazidi kuwa tete, polisi wakikabiliana na makundi ya waasi wenye itikadi kali.

    Soma pia:

  3. Rais wa Taiwan: Hatutakubali kuwa sehemu ya China

    Rais wa Taiwan, Lai Ching-te, amesema Taiwan inapaswa kuja pamoja kulinda demokrasia yake na kuhakikisha haiwi sehemu ya China.

    Lai amewataka wanachama wa chama chake cha Democratic Progressive Party (DPP) kupinga kile alichokiita "hofu nyekundu" inayotoka Beijing.

    Lai, ambaye alishinda uchaguzi miaka miwili iliyopita, pamoja na chama chake tawala cha DPP, wamekuwa wakitetea utambulisho wa kipekee wa Taiwan kuwa taifa huru na kupinga kuwa sehemu ya China.

    Msimamo huo mara kwa mara umeighadhabisha Beijing, ambayo inaiona Taiwan kuwa sehemu ya eneo lake.

    Soma pia:

  4. Bahrain yasema imefaulu kudungua makombora na droni za Iran

    Jeshi la Bahrain limesema limefanikiwa kukabiliana na mashambulizi ya makombora na ndege zisizo na rubani yalirushwa na Iran.

    Katika taarifa yake, jeshi hilo lilisema mifumo yake ya ulinzi wa anga iliweza kuzuia na kuharibu mashambulizi kadhaa ya anga yaliyotekelezwa na Iran siku ya Jumapili.

    Jeshi la Bahrain limesema kuwa matumizi ya makombora na droni kulenga raia na miundombinu ni ukiukaji wa sheria za kimataifa za kibinadamu.

    Aidha, jeshi hilo limewataka wananchi wake kuwa waangalifu, kuepuka kukaribia vitu visivyojulikana au vinavyotia shaka ambavyo vinaweza kuwa mabaki ya mashambulizi hayo.

    Soma pia:

  5. Uhaba wa maji waanza kushuhudiwa Kuwait, baada ya mashambulizi ya Iran

    Shirika la habari la AFP limeripoti ongezeko la mahitaji ya maji na vyakula vya makopo nchini Kuwait.

    Hapo jana, Kuwait iliishutumu Iran kwa kushambulia mtambo wa kuzalisha umeme na kituo cha usambazaji wa maji kwa mara ya pili.

    Mkazi mmoja wa Kuwait aliiambia AFP kuwa kuna wasiwasi kuhusu uwezekano wa upungufu wa bidhaa muhimu endapo mvutano utaendelea.

    “Tangu asubuhi ya leo, mahitaji ya maji na vyakula vya makopo yameongezeka kutokana na hofu ya uwezekano wa kukatika kwa huduma au kuvurugika kwa mifumo ya usambazaji wa maji,” Hassan Rayan, mwenye umri wa miaka 61, aliliambia shirika hilo la habari.

    Ali Mahmoud, raia wa Kuwait mwenye umri wa miaka 46, pia alisema, “Ingawa leo ni siku ya mapumziko, barabara na fukwe za karibu hazina watu.”

    Soma pia:

  6. Urusi yatekeleza shambulio kubwa la makombora mjini Kyiv

    Urusi imetekeleza mashambulizi ya makombora ya balistiki katika mji mkuu wa Ukraine, Kyiv, na kusababisha kifo cha mtu mmoja na kuwajeruhi takriban watu 14.

    Maeneo kadhaa katika mji huo yalilengwa usiku kucha.

    Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelensky, ametaja mashambulizi hayo kuwa “moja ya mashambulizi makubwa zaidi ya makombora ya balistiki dhidi ya Kyiv” tangu kuanza kwa uvamizi wa Urusi nchini humo.

    Jeshi la Ukraine limesema mifumo yake ya ulinzi wa anga ilidungua makombora 18 kati ya 41 yaliyorushwa. Aidha walifanikiwa pia kuzuia ndege zisizo na rubani 108.

    Jeshi la anga la Ukraine limesema mashambulizi ya hivi karibuni dhidi ya Kyiv yamehusisha mifumo mbalimbali ya silaha za Urusi, ikiwemo makombora ya Iskander na makombora ya kasi ya juu ya Zircon, pamoja na droni 125.

    Wazima moto wamekuwa wakipambana na kuzima moto katika maghala mawili yaliyoshambuliwa.

    Soma pia:

  7. Jenerali Moses Ali na mwanasiasa mkongwe Uganda aaga dunia

    Jenerali mstaafu Moses Ali, mmoja wa makamanda wa kijeshi waliodumu kwa muda mrefu zaidi nchini Uganda,na mwanasiasa aliyekuwa Naibu Waziri Mkuu wa zamani, amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 87.

    Binti wa yake, ambaye aliomba jina lake lisitajwe kwa sababu hana mamlaka ya kuzungumza kwa niaba ya familia, alisema mwanasiasa huyo mkongwe alifariki takriban saa kumi jioni hapo jana.

    Moses Ali anaacha nyuma urithi mkubwa na wenye historia tata katika siasa na jeshi la Uganda. Katika kipindi cha zaidi ya miongo mitano ya utumishi wake, alihudumu chini ya serikali mbalimbali zilizofuatana, akaongoza harakati za uasi, akashiriki katika mazungumzo ya amani, na baadaye akarudi kuwa mmoja wa mawaziri waliodumu muda mrefu zaidi katika Baraza la Mawaziri la Uganda.

    Soma pia:

  8. Jeshi la Kuwait lasema linakabiliana na wimbi la mashambulizi ya Iran

    Jeshi la Kuwait limesema linakabiliana na wimbi la mashambulizi ya anga yanayodaiwa kutekelezwa na Iran.

    Katika taarifa yetu ya awali tulikuwa tumeripoti kuwa jeshi la Iran limelenga kambi za Marekani nchini Kuwait.

    Katika taarifa yake, jeshi la Kuwait limesema linakabiliana na "uchokozi wa Iran" na kwamba "mifumo yao ya ulinzi wa anga kwa sasa inaendelea kuzuia mashambulizi ya makombora na droni kutoka kwa adui."

    Shirika la habari la AFP pia limeripoti kuwa ving’ora vya tahadhari vimesikika nchini Kuwait.

    Mashambulizi dhidi ya miundombinu inayohusiana na mitambo ya kusafisha maji ya chumvi, vituo vya umeme, na vituo vya mafuta nchini Kuwait imezua ghadhambu miongoni mwa mataifa ya Ghuba ya Uajemi.

    Baraza la Ushirikiano la Ghuba (GCC) limeandika katika taarifa yake kwamba "mashambulizi ya Iran dhidi ya miundo mbinu ya kiraia katika nchi jirani ni uhalifu wa kivita."

    Soma pia:

  9. Trump kuhudhuria fainali ya Kombe la Dunia

    Rais wa Marekani, Donald Trump, anatarajiwa kuhudhuria fainali ya Kombe la Dunia kati ya Hispania na Argentina hii leo na kuwakabidhi kombe la ushindi timu itakayoibuka mshindi.

    Huu utakuwa mchezo wa kwanza wa Kombe la Dunia ambao Trump atautazama akiwa uwanjani. Mke wake, Melania Trump, pamoja na baba yake Melania, pia wanatarajiwa kuhudhuria mechi hiyo itakayochezwa mjini New Jersey.

    Trump kuhudhuria mechi hiyo kunakuja chini ya wiki mbili baada ya kumpigia simu Rais wa FIFA akitaka marufuku dhidi ya mshambuliaji wa timu ya taifa ya Marekani, Folarin Balogun, iondolewe ili aweze kucheza mechi ya hatua ya 16 bora dhidi ya Ubelgiji. Simu hiyo ilizua hisia na ukosoaji mkubwa kuhusu madai ya kuingiliwa kwa maamuzi ya FIFA na ushawishi wa kisiasa.

    Licha ya utata huo, Trump ameelezea Kombe la Dunia la 2026 kuwa moja ya mashindano ya michezo yaliyofanikiwa zaidi katika historia.

    Akizungumza katika hafla iliyofanyika mjini New York siku ya Ijumaa akiwa pamoja na Rais wa FIFA, alisema mashindano hayo yamechangia kuongeza umaarufu wa soka nchini Marekani.

    Fainali ya Kombe la Dunia kati ya Hispania na Argentina inatarajiwa kuchezwa hii leo.

    Soma pia:

  10. Andrew Tate na ndugu yake wakamatwa nchini Marekani

    Mshawishi na mtengeneza maudhui mwenye utata kwenye mitandao ya kijamii, Andrew Tate, na ndugu yake Tristan Tate, wamekamatwa nchini Marekani baada ya mamlaka za Uingereza kutangaza kuwa zimewafungulia mashtaka mapya.

    Ofisi ya Mashtaka ya Umma ya Uingereza imesema Andrew Tate anakabiliwa na mashtaka saba mapya ya ubakaji pamoja na mashtaka mengine yanayohusiana na madai ya biashara haramu ya binadamu kwa ajili ya unyanyasaji wa kingono na makosa yanayohusiana na picha chafu za watoto.

    Kwa upande wake, Tristan Tate ameshtakiwa kwa kosa moja la unyanyasaji wa kingono, makosa mawili ya ubakaji na makosa matatu ya kupanga au kuwezesha biashara haramu ya binadamu kwa madhumuni ya unyanyasaji wa kingono.

    Mashtaka hayo yanahusiana na madai ya uhalifu unaodaiwa kufanyika kati ya mwezi Julai 2010 na Agosti 2017. Ndugu hao wamekanusha madai yote yanayowakabili.

    Maafisa wa Marekani wameiambia BBC kuwa ndugu hao wanazuiliwa, huku msemaji wa Idara ya Haki ya Marekani akisema kukamatwa kwao kumefanyika kwa mujibu wa taratibu za kuwarejesha nchini Uingereza.

    Wawili hao ni raia wa Uingereza na Marekani

    Soma pia:

  11. Marekani yalenga maeneo ya Shadegan na Kisiwa cha Qeshm nchini Iran

    Vyombo vya habari vya Iran vimeripoti mashambulizi mapya yanayodaiwa kutekelezwa na Marekani katika maeneo ya mikoa ya Khuzestan na Hormozgan.

    Naibu afisa wa usalama katika ofisi ya gavana wa mkoa wa Khuzestan, amesema kuwa ndege za kivita za Marekani zilirusha makombora katika eneo karibu na mji wa Shadegan saa kumi na moja alfajiri kwa saa za eneo hilo.

    Shirika la habari la Tasnim pia liliripoti kuwa majira ya saa kumi na mbili asubuhi, Kisiwa cha Qeshm kililengwa tena na ndege za kivita za Marekani, huku angalau milipuko miwili ikisikika.

    Kulingana na shirika hilo la habari, uchunguzi unaendelea kufanyika kubaini maeneo yaliyolengwa, uharibifu na idadi ya majeruhi.

    Soma pia:

  12. Marekani yaishambulia Iran, baada ya wanajeshi wake kuuawa

    Marekani imeanzisha duru nyingine ya mashambulizi ya anga dhidi ya Iran usiku wa kuamkia leo, ikilenga vituo vya ufuatiliaji eneo la pwani ya Iran na mifumo ya ulinzi wa anga.

    Kituo kikuu cha kuendesha oparesheni za kijeshi cha Marekani CENTCOM kimesema vikosi vyake vilifanikiwa kushambulia uwezo wa kijeshi wa Iran, huku vyombo vya habari vya serikali ya Iran vikidai kuwa Kisiwa cha Qeshm, kilichopo katika Mlango wa Bahari wa Hormuz, kililengwa.

    CENTCOM pia ilisema ililenga Kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu cha Iran (IRGC), ambacho ilikihusisha na shambulio lililosababisha vifo vya wanajeshi wawili wa Marekani nchini Jordan siku ya Ijumaa.

    Mwanajeshi mmoja wa Marekani bado hajulikani alipo.

    Kujibu mashambulizi hayo, jeshi la Iran limetekeleza mashambulizi ya ndege zisizo na rubani dhidi ya kambi mbili za kijeshi za Marekani nchini Kuwait.

    Soma pia:

  13. Hujambo na karibu katika matangazo yetu ya moja kwa moja Jumamosi ya leo