Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Wahouthi wadai kuhusika na shambulio dhidi ya meli za mafuta baada ya Marekani kufanya mashambulizi zaidi dhidi ya Iran

Kundi la Houthi nchini Yemen linasema limezishambulia meli mbili za mafuta za Saudi Arabia katika Bahari ya Shamu, muda mfupi baada ya Marekani kufanya mashambulizi dhidi ya Iran kwa usiku wa 12 mfululizo.

Muhtasari

Moja kwa moja

Lizzy Masinga

  1. Jeshi la Kuwait: Tunakabiliana na mashambulizi ya makombora na ndege zisizo na rubani kutoka Iran

    Jeshi la Kuwait lilitangaza Alhamisi asubuhi kuwa linakabiliana na mashambulizi ya makombora na ndege zisizo na rubani kutoka Iran.

    Mashambulizi hayo, ambayo yaliripotiwa sambamba na mashambulizi ya anga ya Marekani kusini mwa Iran, yalifafanuliwa na mashirika ya habari yenye uhusiano na vyanzo vya kijeshi vya Iran kama "mashambulizi ya ndege zisizo na rubani dhidi ya kambi ya Marekani huko Ali al-Salem."

    Shirika la Habari la Fars pia liliripoti kusikika kwa mlipuko katika bandari ya Aqaba nchini Jordan, lakini vyanzo vingine havikutaja mashambulizi ya aina hiyo.

  2. Kenya yapokea vifaa vya matibabu kutoka India kuimarisha mapambano dhidi ya Ebola

    Kenya imepokea shehena ya kwanza ya tani 4.5 za vifaa vya matibabu kutoka kwa serikali ya India ili kuimarisha uwezo wa nchi hiyo wa kujiandaa na kukabiliana na uwezekano wa mlipuko wa ugonjwa wa Ebola, The Star imeripoti.

    Shehena hiyo ilikabidhiwa rasmi na Kamishna Mkuu wa India nchini Kenya kwa Waziri wa Afya, Aden Duale, katika hafla iliyofanyika siku ya Jumatano.

    Msaada huo ni sehemu ya jitihada pana za India kusaidia nchi za Afrika kuimarisha uwezo wa kuzuia na kukabiliana na milipuko ya Ebola.

    Vifaa vya matibabu vilivyotolewa vinajumuisha vifaa vya kujikinga binafsi (PPE), vifaa vya kusafirisha sampuli za vipimo, vipima joto vya infrared, kinga za uso, viatu vizito za kujikinga, pamoja na vifaa vingine vya kuzuia na kudhibiti maambukizi.

    Shehena ya pili ya msaada wa matibabu inatarajiwa kuwasili Kenya ndani ya siku chache zijazo.

    Wakati wa hafla ya makabidhiano, maafisa walisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa katika kuimarisha mifumo ya afya na kuboresha maandalizi ya kukabiliana na dharura zinazotokana na vitisho vya magonjwa ya kuambukiza.

    Msaada huo unakuja wakati Kenya ikiendelea kuimarisha ufuatiliaji wa magonjwa, maandalizi, na hatua za haraka za kukabiliana na dharura ili kujikinga dhidi ya hatari ya kuenea kwa Ebola kuvuka mipaka na magonjwa mengine mapya ya kuambukiza.

    Unaweza kusoma;

  3. Meya wa New York: Sina mamlaka ya kumkamata Netanyahu

    Meya wa Jiji la New York, Zohran Mamdani, ambaye awali aliahidi kumkamata Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu iwapo angetembelea jiji hilo, sasa amesema hana mamlaka ya kisheria kufanya hivyo.

    Katika video aliyochapisha kwenye mitandao ya kijamii, Mamdani alisema badala yake anatoa wito kwa serikali ya Marekani kuchukua hatua kuhusu hati ya kukamatwa iliyotolewa na Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) dhidi ya Netanyahu kwa tuhuma za uhalifu wa kivita.

    Kisheria, iwapo Netanyahu angeingia katika nchi mwanachama wa ICC, angeweza kukamatwa na kukabidhiwa mahakamani. Hata hivyo, Marekani si mwanachama wa ICC, hivyo haiwajibiki kutekeleza hati hiyo.

    Rais wa Marekani Donald Trump amesema Netanyahu hatakamatwa kwa namna yoyote akiwa nchini Marekani.

    Trump alisema Netanyahu anaendelea kupambana na Iran, ambayo aliituhumu kwa kuhusika na mauaji ya waandamanaji na wanajeshi wa Marekani.

    Kauli hiyo ya Trump ilijibu mahojiano ambayo Mamdani alifanya na gazeti la The New York Times, ambapo alisema alikuwa akifanya mazungumzo na vyombo vya sheria kuhusu uwezekano wa kutekeleza hati ya ICC.

    Hata hivyo, siku iliyofuata Mamdani alisema timu yake ya wanasheria imepitia njia zote zinazowezekana kisheria na kubaini kuwa ofisi ya meya haina mamlaka huru ya kutekeleza hati hiyo.

    Aliongeza kuwa mamlaka hayo yako mikononi mwa serikali ya shirikisho la Marekani, na akaisihi Marekani ijiunge na ICC na kutekeleza hati hiyo ya kukamatwa.

  4. Meli za mafuta zageuza njia ghafla baada ya tishio la Wahouthi dhidi ya usafirishaji wa baharini

    Takribani meli saba za kusafirisha mafuta zimegeuza njia karibu na pwani ya Yemen baada ya kundi la Wahouthi, linalohusishwa na Iran, kutangaza "zuio la baharini" dhidi ya Saudi Arabia siku ya Jumatatu, kwa mujibu wa taarifa za ufuatiliaji wa meli.

    Meli zote zilikuwa zikielekea au zikitoka katika bandari za Saudi Arabia, lakini zilibadili ghafla mwelekeo baada ya tangazo hilo.

    Takriban asilimia 15 ya biashara ya baharini duniani hupitia Bahari ya Shamu, ambayo inaunganisha Bahari ya Mediterania na Ghuba ya Aden kupitia njia mbili muhimu: Mfereji wa Suez nchini Misri na Mlango wa Bab al-Mandab kati ya Yemen na Pembe ya Afrika.

    Bahari ya Shamu imekuwa njia muhimu ya usafirishaji wa mafuta ya Saudi Arabia tangu vita kati ya Marekani, Israel na Iran visababishe kuzorota kwa usafiri kupitia Mlango wa Hormuz, hali iliyopunguza kwa kiasi kikubwa usafirishaji wa mafuta na gesi kutoka Ghuba ya Uajemi.

    Mchambuzi Rosemary Kelanic wa taasisi ya Defense Priorities nchini Marekani amesema njia ya Bahari ya Shamu imekuwa na mchango mkubwa katika kupunguza shinikizo kwenye masoko ya dunia, na ikiwa Wahouthi watazuia zaidi biashara ya baharini, bei za mafuta zinaweza kupanda.

    Kwa mujibu wa kampuni ya ujasusi wa masuala ya baharini ya Kpler, siku moja kabla ya Wahouthi kutangaza zuio hilo, meli 20 ziliingia Bahari ya Shamu na meli 22 zilitoka kupitia Mlango wa Bab al-Mandab.

    Kelanic ameambia BBC Verify kuwa iwapo Wahouthi wataendelea kushambulia meli katika Bahari ya Shamu au Ghuba ya Aden, hali hiyo itaathiri usafiri wa kimataifa kwa ujumla, si meli zinazoelekea Saudi Arabia pekee.

    Wakati huo huo, kikosi cha majini cha Umoja wa Ulaya kilitoa ushauri siku ya Jumatano kikizitaka meli za kibiashara zinazohusishwa na maslahi ya Israel, Marekani au Saudi Arabia kuepuka kupita Bahari ya Shamu na Ghuba ya Aden hadi kiwango cha tishio kitakapopungua.

    Unaweza kusoma;

  5. Marekani inachunguza uwezekano wa msaada wa Urusi kwa Iran kulenga vituo vya CIA

    Reuters iliripoti katika ripoti ya kipekee, ikinukuu vyanzo vyenye taarifa, kwamba Marekani inachunguza kama Urusi ilihusika katika mashambulizi ya ndege zisizo na rubani za Iran dhidi ya vituo vya Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA) katika nchi za Ghuba ya Uajemi.

    Kulingana na vyanzo hivi, uchunguzi wa Marekani bado unaendelea na maafisa wa Marekani wanatathmini ushahidi na taarifa zilizopo kuhusu uwezekano wa Urusi kuhusika katika mashambulizi haya.

    Maelezo rasmi ya vituo vinavyolengwa na CIA katika eneo hilo hayajatolewa. Ikulu ya White House na Pentagon hazijatoa habari yoyote kuhusu kulengwa kwa nafasi zao katika eneo hilo au majeruhi au hasara za kijeshi katika miezi minne iliyopita, na hata zimeagiza satelaiti za kibinafsi kudhibiti na kutochapisha picha za angani.

    Nchi katika eneo hilo pia zimezuia na kudhibiti vikali ufikiaji huru wa vyombo vya habari na hata uwasilishaji wa ripoti za umma kutoka maeneo yaliyolengwa, na zimezuia uvujaji wa habari kwa adhabu kali - katika baadhi ya matukio hata tishio la adhabu ya kifo.

  6. Wahouthi wadai kuhusika na shambulio dhidi ya meli za mafuta baada ya Marekani kufanya mashambulizi zaidi dhidi ya Iran.

    Kundi la Houthi nchini Yemen linasema limezishambulia meli mbili za mafuta za Saudi Arabia katika Bahari ya Shamu, muda mfupi baada ya Marekani kufanya mashambulizi dhidi ya Iran kwa usiku wa 12 mfululizo.

    Vyombo vya habari vya serikali ya Iran viliripoti kuwa watu wawili waliuawa katika mashambulizi ya Marekani siku ya Jumatano, na kwamba meli moja ya mafuta ilishika moto kufuatia mlipuko katika njia yenye mabomu ya majini kwenye Lango la Hormuz.

    Kabla ya mfululizo huo wa hivi karibuni wa mashambulizi, Rais wa Marekani Donald Trump alikuwa ametishia kuharibu daraja au kituo cha kuzalisha umeme cha Iran iwapo nchi hiyo ingeshambulia meli katika lango hilo, na pia "kushughulikia" kundi la Houthi iwapo lingezuia usafiri katika Bahari ya Shamu.

    Iwapo itathibitishwa, shambulio hilo la Houthi litakuwa la kwanza tangu kundi hilo linaloungwa mkono na Iran litangaze "vikwazo vya usafiri wa baharini" dhidi ya Saudi Arabia. Kundi la Houthi lilitaja meli hizo kuwa ni *Encelia* na *Layla*, ingawa hakuna uthibitisho rasmi kuhusu kuhusika kwao au shambulio dhidi ya meli ya *Layla*.

    Msemaji wa kijeshi wa kundi hilo, Yahya Saree, alisema walizilenga meli hizo kwa kutumia ndege zisizo na rubani (drones) na makombora kwa madai ya kukiuka zuio lao la usafiri wa majini. Saree aliongeza kuwa kundi la Houthi limeahidi kuendeleza operesheni zake za majini na kuendelea "kutekeleza mkakati wa 'kuzingirwa kwa '" (kulipiza kisasi kwa hatua kama hiyo).

    Shirika la Uingereza la Operesheni za Biashara ya Baharini (UKMTO) liliripoti kuwa "kitu kisichojulikana kilichorushwa" kiligonga meli ya mafuta ya Saudi Arabia umbali wa takriban kilomita 130 kutoka Al Shuqaiq nchini Saudi Arabia saa 20:00 kwa saa za GMT. Shirika hilo lilisema shambulio hilo lilisababisha moto lakini hakukuwa na majeruhi au vifo.

  7. Hujambo na karibu katika taarifa zetu za moja kwa moja