Takribani meli saba za kusafirisha mafuta zimegeuza njia karibu na pwani ya Yemen baada ya kundi la Wahouthi,
linalohusishwa na Iran, kutangaza "zuio la baharini" dhidi
ya Saudi Arabia siku ya Jumatatu, kwa mujibu wa taarifa za
ufuatiliaji wa meli.
Meli zote zilikuwa zikielekea au zikitoka katika
bandari za Saudi Arabia, lakini zilibadili ghafla mwelekeo baada
ya tangazo hilo.
Takriban asilimia 15 ya biashara ya
baharini duniani hupitia Bahari ya Shamu, ambayo
inaunganisha Bahari ya Mediterania na Ghuba ya
Aden kupitia njia mbili muhimu: Mfereji wa Suez nchini
Misri na Mlango wa Bab al-Mandab kati ya Yemen na
Pembe ya Afrika.
Bahari ya Shamu imekuwa njia muhimu ya
usafirishaji wa mafuta ya Saudi Arabia tangu vita kati ya
Marekani, Israel na Iran visababishe kuzorota
kwa usafiri kupitia Mlango wa Hormuz, hali iliyopunguza
kwa kiasi kikubwa usafirishaji wa mafuta na gesi kutoka
Ghuba ya Uajemi.
Mchambuzi Rosemary Kelanic wa taasisi ya Defense
Priorities nchini Marekani amesema njia ya Bahari ya Shamu
imekuwa na mchango mkubwa katika kupunguza shinikizo kwenye
masoko ya dunia, na ikiwa Wahouthi watazuia zaidi biashara
ya baharini, bei za mafuta zinaweza kupanda.
Kwa mujibu wa kampuni ya ujasusi wa masuala
ya baharini ya Kpler, siku moja kabla ya Wahouthi
kutangaza zuio hilo, meli 20 ziliingia Bahari ya Shamu
na meli 22 zilitoka kupitia Mlango wa Bab al-Mandab.
Kelanic ameambia BBC Verify kuwa iwapo Wahouthi
wataendelea kushambulia meli katika Bahari ya Shamu au Ghuba
ya Aden, hali hiyo itaathiri usafiri wa kimataifa kwa
ujumla, si meli zinazoelekea Saudi Arabia pekee.
Wakati huo huo, kikosi cha majini cha Umoja wa Ulaya kilitoa ushauri siku ya Jumatano kikizitaka meli za
kibiashara zinazohusishwa na maslahi ya Israel, Marekani au Saudi Arabia
kuepuka kupita Bahari ya Shamu na Ghuba ya Aden hadi kiwango cha tishio
kitakapopungua.